Best Blogger TipsSoon

Mittwoch, 15. Juni 2011

TZMPAKAAU

  Bungeni sasa ni vuta ni kuvute
  • Makinda akolikoroga
  • Mbunge wa NCCR atimuliwa bungeni
  • Zitto wa CHADEMA aendelea kukomaa na posho

Spika wa bunge Anna makinda
Kauli ya Spika wa Bunge, Anne Makinda, iliyotafisriwa kama ni kuwabeza watu wa Kariakoo, eneo maarufu kwa biashara jijini Dar es Salaam, jana ilimlazimu kiongozi huyo kuomba radhi.

Makinda akitoa matangazo na ufafanuzi wa masuala mbalimbali bungeni jana, kwanza akieleza kusikitishwa kwake na mwenendo wa wabunge ndani ya Bunge kwa kufanya mambo kinyume cha kanuni zinazokubalika, alifananisha hali hiyo na kama watu wako Kariakoo.
Waziri wa uchukuzi Omari Nundu

Awali Makinda alisema kuwa alichokuwa amefanya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Rasmi Bungeni, Freeman Mbowe, kwa kutaka mwongozo wa Spika baada ya kupata majibu yasiyoridhisha kutoka kwa Waziri wa Uchukuzi, Omari Nundu, alikuwa sahihi na si kama wanavyofanya wabunge wengine wanaopiga tu kelele za kuomba mwongozo wa Spika wakati mzungumzaji akiwa bado anaendelea kuzungumza kama wako Kariakoo.
Mwenyekiti wa CHADEMA na mbunge wa hai Freeman Mbowe
Makinda alisema kimsingi, mwongozo wa Spika unaombwa mara tu baada ya tukio husika kumalizika ndani ya Bunge, kama ambavyo alikuwa amefanya Mbowe.

Mbowe alisema katika majibu ya waziri juu ya ujenzi wa njia ya kurukia ndege katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro (KIA) alikuwa amepotosha kwa kusema kuwa fedha za ujenzi zilikuwa zimetolewa na aliyekuwa mwekezaji wa uwanja huo.

Mbowe alisema ukweli ni kwamba fedha za ujenzi huo Dola za Marekani milioni nne, zilitolewa na Benki ya Dunia na kujengwa na kampuni ya Federitsi, kwa maana hiyo alimuomba Spika amtake Waziri aondoe majibu ya swali hilo katika hansard za Bunge.

Hata hivyo, Makinda alimtaka Mbowe kuwasilisha kwa maandishi hoja yake ili iweze kufanyiwa kazi kwa kuwa hakuwa na majibu ya papo kwa papo kama ni nani alikuwa sahihi kati yake na Waziri.
Ni katika muktadha huo, Spika aliwataka wabunge kuacha mambo ya ovyo wanapokuwa katika vikao vya Bunge kwani wanatia aibu kwa watu wanaowatazama na wameligeuza Bunge kama Kariakoo.
Vile vile, aliwaasa wasome vizuri bajeti ili watakapochangia wachangie vitu vya msingi badala ya kuzungumza mambo yasiyohusu bajeti.
Baada ya malekezo hayo aliyotoa jana baada ya kipindi cha maswali na majibu kabla wabunge hawajaanza kujadili mpango wa miaka mitano, pia alieleza jinsi alivyosikitishwa na kikao cha juzi jioni.

Kushoto ni mzee Kingune Ngombare Mwiru na kulia ni Simbachamwene

Alisema alisikitishwa na hali iliyotokea juzi katika kikao cha jioni kilichokuwa kikiongozwa na Mwenyekiti wa Bunge, Mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene.
Alisema katika kikao hicho wabunge walifanya vituko vya ajabu kiasi cha yeye (Makinda), kushindwa kuendelea kuangalia mwenendo wa kikao hicho.
“Hii ni aibu kubwa na sijui kwa nini mnajidharaulisha kwa wananchi, mnajua watu huko nje wanawaheshimu sana, sasa mkifanya mambo ya ovyo wanawadharau na mjue haya yote yanayofanyika humu yanaonekana, mimi mwenyewe nilikuwa naangalia, lakini nikashindwa kuendelea kwani nilikuwa naona vitu vya ajabu ajabu,” alisema Makinda na kuongeza kuwa:
“Hapa bungeni kuna utaratibu wa kuzungumza, mtu akiwa anazungumza wengine mnapaswa kumsikiliza, lakini jana (Juzi) mtu mmoja anachangia na wengine wanazungumza utadhani mko Kariakoo.”
Katika kikao cha juzi jioni, kilichoongozwa na Simbachawene, wabunge walikuwa wakiwasha vipaza sauti vyao na kutoa maneno ya vijembe kwa wenzao na wengine wakizomea wachangiaji. Hali hiyo ilimpa wakati mgumu Simbachawene, ambaye alikuwa akilazimika kuwakatisha wabunge waliokuwa wakiomba mwongozo ili kuwabana wazungumzaji walioonekana kuwakejeli wengine.
“ Waheshimiwa wabunge tutumie muda wetu kujadili huu mpango ulio mbele yetu, nikiruhusu kila mtu asimame atoe mwongozo muda wote tutakuwa tumeupoteza bure, naomba tuwe makini,” alisema Spika Makinda.
Ukiliona hili jengo unajua umefika ....hapa ni Kariakoo.

Baada ya kurusha kombora kwa watu wa Kariakoo, mchana Makinda alilazimika kuomba radhi kutokana na tafsiri iliyoonekana kuwakera baadhi yao.
Kauli kwamba wabunge wasizungumze kama wako Kariakoo ilionekana kuwakera baadhi ya watu waliomtumia ujumbe wakimweleza kuwa amewadhalilisha na kwa kuonyesha kuwa eneo hilo halina maana.
“Nawaomba radhi waliokwazika na kauli yangu, lakini sikumaanisha kuwadharau watu wa Kariakoo, nilichokuwa na sema ni kwamba watu watofautishe kati ya kuzungumza bungeni na mitaani, hapa bungeni kuna taratibu zake za kuzungumza, mtu mmoja akizungumza wengine mnapaswa kumsikiliza tofauti na sehemu kama sokoni Kariakoo ambapo mtu mmoja anaweza kuwa anazungumza na wengine wanazungumza wakati huo huo.

Keine Kommentare:

Kommentar veröffentlichen